MIMI NITAKULINDA.




Na Lucy Patrick

Naombeni nilindwe nisiuawe nami niweze kutimiza ndoto yangu ya kuwa mwalimuHaya ni maneneo ya Mtoto mdogo wa miaka mitatu Princess Suo ambaye ni mlemavu wa ngozi yaani Albino.

Nimaneno yanayotia uchungu  huzuni sana hasa kwa nchi kama Tanzania ambayo inajulikana duniani kote kama kisiwa cha amani hivi amani  hiyo iko wapi?


Kama mtanzania unajisikiaje kuona vitendo vya kikatili kama kuuawa kwa Albino,kukatwa viungo na kubaki na ulemavu wa kudumu vikiendelea majibu unayo mwenyewe chukua hatua kuwa mlinzi kwa watu wenye ulemavu 


Inaumiza sana kuona wenzetu wakiishi maisha yasiyo na amani katika nchi yao wenyewe tutaendelea kusema Kwa nguvu zote tunaumia sana na hii hali  kuona wenzetu wakiwwa wanauawa kama wanyama mpaka lini lazima tuchukue hatua kuhakikisha ndugu zetu hawa wanaishi kwa amani na kufurahia uubwaji wao lazima tukumbuke kuwa wao ni kama binadamu wengine tu hizi imani za kwamba wao ni dili hazina manufaa yoyote kwetu.

“Hata sijui niongee nini ila dah mmevuka mipaka sasa hivi Mh Rais Dr Jakaya Mrisho Kikwete hivi ni kweli hamuwajui wauwaji au?? Maana kila nikikaa hainiingii akilini hivi hao wauwaji wana utaalam gani wa serikali kushindwa kuwatia mkononi au mnataka tuwafikirie nini jamani kwamba mnahusika au?”
“Au hii sio issue ya kitaifa mkaichukulia mkazo kama mnavyochukulia zingine ,” alihoji Keisha.
” Inaniuma sana na ninakata tamaa na nchi yangu kila siku zinavyozidi kwenda    natamani niiikimbie hii nchi niende mbali ambapo labda sitoweza kushuhudia huu ukatili unaoendelea ndani ya nchi mnayoiita nchi yenye amani.”
“Maisha yetu yapo hatarini Mh Raisi sijawahi kujutia kuzaliwa hivi am always proud na nilivyo lakini this time aahh ee mungu Nisamehe mja wako kwa mara ya kwanza najutia kuwa na hii hali.”Hayo ni maneno ya Msanii  wa bongo flavor  Keisha ambaye naye pia ni Albino .


Kwa hali ya kawaida ukisoma maneno kama hayo ambayo yanaumiza sasa imefika hatua ya kusema imetosha sasa lazima liwe jukumu letu sote kwa umoja wetu kama watanzania tuseme kwa pamoja inatosha sasa na kuwalinda ndugu zetu albino.



Ipo haja kubwa kama taifa tukiwa katika mchakato wa kupata katiba mpya kuhakikisha sheria inafanyiwa ukarabati mkubwa kwenye vipengele ambavyo  vinachelewesha  hukumu za kesi ya mauaji ya Albino na badala yake kesi hizo ziweze kuharakishwa  na mtuhumiwa aweze kupewa adhabu kali. Kwa kufanya hivyo kunauwezekano wa kupunguza ama kutokomeza kabisa matukio ya mauaji ya albino hapa nchini . 



Kwa mujibu wa  Bwana Joseph Tona ambaye ni Rais wa Chama cha Albino Tanzania matukio zaidi ya 120 ya kesi za mauji ya albino, kati yake 11 ndiyo yaliyofikishwa Mahakama, ambapo kati ya hizo kesi tano tu zimeweza kutolewa hukumu hadi sasa.Kwa hiyo tunaweza kuona  uwiano jinsi kesi hizo zinavyokwenda kwa kasi ndogo huku mauaji haya yakiendelea.


Mauaji haya yanayoendelea yanaichafua nchi yetu ambapo tumeona tamko la Kamishna wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa (UN), Zeid Ra’ad Al Hussein, kuitaka  Serikali ya Tanzania kuchunguza na kuwashtaki watu waliohusika na uhalifu wa mauaji dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino).


“Nalaani vikali mauaji haya ya kutisha na ukataji viungo vya Yohana Bahati, mtoto albino mwenye umri wa mwaka mmoja kaskazini mwa Tanzania, Yohana alitekwa kutoka kwa mama yake na watu watano wasiojulikana waliokuwa na silaha za jadi, na kumjeruhi kwa mapanga mama yake alijeruhiwa vibaya wakati akijaribu kumwokoa mwanae”alisema Zeid Ra’ad Al Hussein 

 Mwili wa mtoto huyo uliokotwa Februari 17 ukiwa hauna mikono wala miguu.
Al Hussein, alisema mashambulizi dhidi ya albino, mara nyingi huchochewa na matumizi ya viungo vyao vya mwili kwa ajili ya ushirikina, ambapo hadi sasa yamegharimu maisha ya watu 76 nchini Tanzania tangu mwaka 2000.


Bado watu wengi wamekuwa wanahoji ongezeko la vitendo vya mauaji ya Albino kujitokeza kipindi cha uchaguzi ambapo tunashuhudia karibu kila mwaka wakati tukikaribia uchaguzi mkuu ndipo vitendo vya namna hii ya ukatili  hujitokeza kwa kasi  kuna nini kimejificha hapo.


Wakati nakua nilikuwa Napata kusimuliwa kuwa albino huwa hawafi bali wanapotea tu na mimi niliamini hivyo na nina imani wengi story hii mliisikia.Hili jambo la kupotea tu limenifanya kutafakari kwa upya kuwa kuna uwezekano albino walikuwa wakiuawa toka zamani kwa siri hivyo watu wakiwa hawawaoni wanasema wametoweka kumbe kuna uwezekano mkubwa walikuwa wanauawa kwa imani hizi za ushirikina na jamii ilikuwa haielewi jambo hili.


Kwa upande wenu viongozi mbona kuna ukimya katika hili tumeshuhudia wasanii na watu mbalimbali wakikemea na kupinga ukatili huu katika mitandao mbalimbali ya kijamii lakini hali ni tofauti kwa viongozi wetu swali ni kwanini mko kimya? je ukimya wenu ni kwamba mnaunga mkono jambo hili au ndio mnaunda tume ya uchunguzi.



Tumeshuhuda mkiwa wepesi kupinga nguvu zote Suala la Escrow,,EPA na mengineyo je ni kwamba hili haliwasumbui na hamuoni kama wananchi wanawatazama ninyi mbona wepesi ule tulio uona katika mambo ya ufisadi hatuuoni katika hili la mauaji ya Albino au ninyi sio wawakilishi wao  jitafakarini.



Mauaji haya yamekuwa yakiongezeka  siku hadi  siku ambapo katika Maadhimisho ya Siku ya Amani Kimataifa ya mwaka jana 2014 Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu Tanzania (Shivyawata), limeitaka serikali kupitisha adhabu ya kunyongwa kwa wale wanaohusika na mauaji ya Albino.



Mimi naamini walikuwa sawa maana tunaambiwa utamu wa ngoma sharti uingie ucheze.Imani yangu ni kwamba kama mambo haya ya ukatili yangemkuta mmoja kati ya viongozi wetu labda mngeamka na kuanza kuwatetea na kuwalinda albino lakini kwa sababu hamna uchungu nalo hamuwezi kujua ni maumivu kiasi gani wanayapitia ndugu zetu hawa.


 Kadhalika, takwimu za kutoka mwaka 2006 zinaonyesha kuwa Albino 74 na sasa 76 akiwemo  mtoto Yohana Bahati aliyeuawa hivi karibuni wameshauawa kikatili, huku 56 wakinusurika kifo, na kati yao 11 wameongezewa ulemavu mwingine wa kudumu kwa kukatwa viungo vyao.


Hali hii kwa sasa inawafanya watu wenye aina hii ya ulemavu wa ngozi kuathirika kisaikolojia na kupata msongo wa mawazo pamoja na kuishi kwa mashaka,wasiwasi,woga,kutojiamini na kufichwa kwa kuhofia usalama wao maana hawana amani kabisa katika nchi yao wenyewe,  imefika wakati mimi na wewe kuchukua jukumu la kuwalinda ili tuweze kutokomeza ukatili huu.



Tukiwa tunaelekea uchaguzi mkuu picha hii inaashiria nini hili ni swali ambalo tunatakiwa kujiuliza kuna mahusiano gani kati ya hivi vitu viwili imekuwa ikisemekana waganga wa jadi kutumiwa na na viongozi wa kubwa katika kuwania nyadhifa mbalimbali serikalini.


 Suala hili inaonekana ni mambo ya ushirikina yanahusishwa hapo lakini pia kwa upande wa serikali haiamini mambo ya ushirikina je ndio sababu ya ukimya wao, lakini wanashuhudia na kuona mauaji hayo hatua gani Serikali imeshachukua ukimya hausaidii ndio maana naona imefika wakati kama jamii kulitazama hili kwa jicho la tatu na kuwalinda Albino.

Japokuwa Tanzania inasifika ndani na nje kama kisiwa cha amani, tafsiri hiyo ni kinyume kwani ni miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa mauaji ya kikatili, hivyo mwito wangu kwa viongozi wa dini tumieni midomo yenu kupinga hali hii kwa sababu na sisi tumeumbwa na Mungu na tunastahili kuisha kama wengine,” alisema  Mariam Stanford, mkazi wa Ngara, mkoani Kagera, ambaye yeye ni muathirika wa janga hili na mikono yake miwili imekatwa .


Nakumbuka mwaka 2009  Serikali kupitia waziri mkuu Mkuu Mizengo Pinda alitoa kauli ya kupiga marufuku leseni za waganga wa kienyeji na wale wa jadi mkakati huu uliishia wapi na ule mpango wa kura za siri zilizopigwa toka mwaka huo wa 2009 hadi sasa ziko wapi mbona mpaka sasa hakuna mrejesho wowote.



Ikitokea mambo kama ya maandamano tumeona jeshi la polisi likitumia nguvu kubwa katika kudhibiti kwanini nguvu hiyo msiihamishie kwenye mauaji na ukatili kwa albino ili kutokomeza hilo. 

Mbona katika suala la vita juu ya madawa ya kulevya tumeona jinsi ambavyo mmeweza kupambana nayo mpaka sasa tunaamini vita hiyo iko mbioni kumalizika kigugumizi cha nini katika hili chukueni hatua ili imani ya albino kwa serikali yao irudi maana kwa sasa hawana imani na mtu yeyote wanahisi kila mtu ni adui kwao na hivyo hawako salama.



Pia kwa taasisi zilizopewa jukumu la kusimamia vitendo hivyo vya kikatili dhidi ya walemavu hususani albino  mnatakiwa kutekeleza majukumu mliyopewa kisheria kwa uadilifu mkubwa jamii ya Watanzania ione haki inatendeka ili kudumisha amani ya nchi.


Hata hivyo Sipingi juhudi za serikali katika mapambano dhidi ya mauaji haya kwa albino ila nafikiri wakati umefika sasa kama jamii kushiriki moja kwa moja kuhakikisha mapambano haya yanaendelea na ukatili dhidi ya albino unaisha kabisa maana naamini katika usemi wa umoja ni nguvu na utengano ni dhaifu kwa pamoja tunaweza.


Simama nami kutokomeza ukatili kwa Albino wasiishi kwa hofu na mashaka katika nchi yao wenyewe.

Mwisho.


Simu:0754884531/0717696330
Email:lucypatrick.e@gmail.com
Blog: www.lucypatickm.blogspot.com.
Previous
Next Post »