Kiongozi wa maharamia astaafu Somalia



Kiongozi mmoja wa kijamii nchini Somalia, ameiambia BBC kuwa, mtu mmoja ambaye ametanjwa na Umoja wa Mataifa, kuwa kinara wa utekaji nyara, ametangaza kuwa amestaafu rasmi kutoka kwa uharamia.

Mohamed Abdi Hassan, ambaye anajulikana kwa jina la utani kama "afweyneh" ikiwa na maan mtu mwenye usemi mkubwa nchini Somalia, amewaambia waandishi wa habari kuwa anastafu kutoka kwa biashara hiyo baada ya miaka minane.



Bwana Hassan aliyasema hayo katika kikao kilichofanyika mjini Abado, kati kati mwa Somalia, eneo ambalo maharamia hao wamekuwa wakiwazuilia mateka wao.

Ulinzi umeimarishwa Somalia


Mashambulio ya kiharamia katika pwani ya Somalia, yalipungua kwa kiasi kikubwa mwaka uliopita.

Baadhi ya maharamia waliokamatwa

Wachanganuzi wanasema hali hiyo iliyokana na kuongezeka kwa meli za kijeshi zinazoshika doria katika eneo hilo na pia kujumuishwa kwa walinzi wanaosindikiza meli za mizigo.

Afisa mkuu wa utawala katika eneo hilo amesema kuwa maharamia wengine katika eneo hilo wamekubali kusalimisha silaha zao.

''Tumewashawishi wao kutomiliki silaha na pia kusalimisha zile wanazomiliki ikiwa ni pamoja na mashua na silaha'' Alisema Bwana Mohamed Adan, ambaye ni kiongozi wa Utawala katika eneo hilo la Adado.

'' Wao wamegundua kuwa kwa sasa hawawezi kuendeleza uharamia kama ilivyokuwa hapo awali bila kuzingatia sheria na pia Uharamia kwa sasa haina faida kama ilivyokuwa'' Aliongeza afisa huyo wa utawala.

Ripoti ya Umoja wa Mataifa


Moja ya meli iliyokuwa imetekwa nyara

Kundi moja la uchunguzi la Mataifa liliripoti mwaka uliopita kuwa Bwana Afweneh, ni mmoja wa watu mashuhuri zaidi kwa mtandao wa uharamia wa Hobyo-Harardhere.

Imeripotiwa kuwa rais mmoja wa zamani wa nchi hiyo alimhaidi hadi ya kibalozi na pia kumkabithi pasi ya kusafiria ya kibalozi ili kuachana na uharamia.

'' Baada ya kushirikia katika vitendo vya uharamia kwa zaidi ya miaka minane, nimeamua leo kuachana nayo na kuanzia hii leo, nitashiriki katika harakati za kupambana makundi ya kiharamia katika pwani ya Somalia'' Shirika la habari la AFP lilimnukuu Bwana Afweyneh.

Kwa mujibu wa shirika hilo la habari, mtandano wake wa uharamia ulihusika na utekaji nyara wa meli ya MV Faina, ya Ukraine mwaka wa 2009, ambayo ilikuwa imebeba magari ya kivita na silaha kutoka urusi.

Meli hiyo iliachiliwa huru baada ya kundi hilo kulipwa kikombozi ya dola milioni tatu nukta mbili, baada ya miezi kadhaa ya majadiliano.
Previous
Next Post »