Taylor anasema kuwa hukumu aliyopewa haifai
Rais wa zamani wa Liberia Charles Taylor, anatarajiwa kuanza
kukataa rufaa katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita huko Hague.
Mwezi Mei mwaka jana, mahakama ilimhukumu miaka hamsini gerezani kwa kusaidia
waasi kufanya vitendo vya kukiuka haki za binadamu, katika nchi jirani ya Sierra
Leone wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe kati ya mwaka 1991 na 2002.
Mawakili wa Taylor, waliitaja hukumu hiyo kama hujuma dhidi ya haki na kuomba
hukumu yenyewe kutupiliwa mbali.
Wakati huohuo,Taylor mwenye umri wa miaka 64, amewaomba wabunge kumlipa
malipo yake ya uzeeni ambayo ni dola
25,000.
Alilaani vikali, hatua ya wabunge kutomlipa malipo yake akisema ni ukiukwaji
mkubwa wa haki yake. Taylor alinukuliwa kwenye barua hiyo akisema kuwa anapaswa
kuruhusiwa huduma za kidiplomasia akiwa gerezani akiongeza kuwa amenyimwa haki
hiyo.
Taylor ndiye alikuwa rais wa kwanza wa zamani Afrika kuhukumiwa kifungo
gerezani, kwa uhalifu wa kivita tangu kesi za wahusika wa utawala wa NAZI baada
ya vita vya pili vya dunia.
Taylor aliwaunga mkono waasi katika vita vya Siera
Leone
Wakati wote kesi ya Taylor ilipokuwa inasikilizwa, alisisitiza kutokuwa na
hatia.
'Ukatili mkubwa'
Mahakama ya Hague iliundwa mwaka 2002 kuwahukumu wale waliohusika pakubwa na
vita vya Sierra Leone ambapo takriban watu 50,000 waliuawa.
Ilimpata na hatia Taylor, kwa makosa 11 ya uhalifu wa kivita, yakiwemo mauaji
na ubakaji na kutajwa kama mojawapo ya uhalifu wa kinyama kuwahi kufaywa
duniani.
Ili aweze kupewa almasi zilizotokana na vita, Taylor aliwapa waasi, msaada wa
silaha na usafiri pamoja na kuwapa moyo kuendelea kupigana hali iliyochochea
vita na mateso dhidi ya watu.
Mawakili wake wanasema kuwa wanakata rufaa kwa misingi 42 wakiteta kuwa
uchunguzi wa jopo lililosikiliza kesi yake haukuweza kuthibitishwa.
Viongozi wa mashtaka hata hivyo wanatarajiwa kusema kuwa mahakama ilifanya
makosa kwa kumhukumu Taylor peke yake na kukosa kuchukulia hatua waasi
alioshirikiana nao.
EmoticonEmoticon