Chavez arejea Cuba kwa matibabu


Rais wa Venezuela, Hugo Chavez leo amerejea nchini Cuba kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji mwingine baada ya madaktari kugundua kuwa ugonjwa wa saratani umemrudia tena.

 Aidha, kwa mara ya kwanza Rais Chavez amemteua mrithi wake katika ishara kwamba ugonjwa wake huenda ukamlazimisha kuachia madaraka.

Wafuasi wake ambao wameshtushwa na kuhuzunishwa na taarifa hizo wamejiandaa kukusanyika kwenye viwanja vikuu vya mji katika nchi hiyo nzima ya Amerika ya Kusini.

 Chavez mwenye umri wa miaka 58, amewaambia wafuasi wake wamchague Makamu wa Rais, Nicolas Maduro iwapo uchaguzi mpya utafanyika.

Akizungumza na vyombo vya habari jana usiku, Chavez amesema ni muhimu afanyiwe upasuaji mwingine na kwa uwezo wa Mungu upasuaji huo utafanikiwa kama ile iliyotanguliwa.

 Rais Chavez tayari amefanyiwa upasuaji wa saratani mara tatu tangu mwezi Juni mwaka 2011.
Previous
Next Post »