Mursi afuta tamko la kujilimbikizia madaraka


Kundi kubwa la upinzani nchini Misri, limesema kuwa hatua ya Rais Mohammed Mursi kufuta tamko lake la kujilimbikizia madaraka zaidi, 
haujafikia matarajio yanayotakiwa ili kumaliza mzozo uliopo nchini humo.

Jana Rais Mursi alitangaza kufuta agizo lake la kujilimbikizia madaraka zaidi unaozifanya mahakama kushindwa kutengua maamuzi yake, ambao alilitoa Novemba 22, mwaka huu.

Hata hivyo, ametangaza kuwa kura ya maoni kuhusu katiba mpya itaendelea kama ilivyopangwa tarehe 15 ya mwezi huu. Afisa wa juu wa muungano wa upinzani wa National Salvation Front, amesema madai yao makubwa ni kuahirishwa kwa kura ya maoni na kushindwa kutimiza madai hayo kutasababisha mapambano zaidi.

Upinzani umerudia kusema kuwa katiba hiyo iliyoandaliwa na jopo linaloongozwa na chama chenye itikadi kali za Kiislamu, inapuuzia uhuru binafsi na haki za wanawake. Makundi makubwa ya upinzani yamesusia mazungumzo ya kumaliza mzozo huo nchini Misri na yamewataka wafuasi wao kuendeleza maandamano.
Previous
Next Post »