Waliofanikiwa Hawaishi Kwenye Sayari Ya Proxima Centauri.


Na: Meshack Maganga- GoBig,Iringa
Ni ukweli usiopingika kwamba Binadamu wanaoitwa  Wamefanikiwa hawaishi kwenye Sayari ijulikanayo kama  Proxima Centauri  Kwa Waliokimbia Umande kama mimi,  proxima Centauri ni sayari mpya iliyogunduliwa siku za karibuni na wanasayansi ina umbo linalokaribiana na duniani yetu na inakadiliwa kuwa ipo umbali wa kilomita tilioni 40 kutoka duniani.

Achana na Jupiter na hiyo Proxima Centauri.

Nimesema kwamba waliofanikiwa hawaishi kwenye Sayari hizo za mbali. Tupo nao kwenye hii Dunia yaani mtaani kwetu na  tupo nao kwenye  Jumuia mbali mbali za kimtaa, kata,wilaya,mkoa, Taifa na kimataifa.

Kama wao wamefanikiwa basi na sisi tunaweza kufanikiwa. Katika kila mwendo wa dunia ama katika kila kipindi cha maisha ya mwanadamu kumekuwepo na matajiri na maskini. Tangu enzi za ZAMA ZA KATI ZA MAWE Kumekuwepo na Matajiri na maskini. Kumekuwepo na waliofanikiwa na wanaoendelea kufanikiwa na kumekuwepo na wapiga kulele na walalamikaji wa miaka yote.

Miaka Ya Hivi karibuni kumekuwepo na Abracadabra ambazo zimepumbaza wengi.  Abracadabra hizi zimewakumba wengi maana zimekuja kwa sura tofauti za kidini, kiutamaduni na kiuchumi. Abracadabra hizo zimesababisha wanadamu wengi wake kwa waume waamini kwamba, ukitaka kufanikiwa lazima uwe Freemason, ama uende kwa Mganga na walogaji ndio upate utajiri.

Kuna Abracadabra nyingine tunazifuata wenyewe ama kwa sababu ya njaa ama mtu akikosa ajira ama  kutaka mafanikio ya haraka haraka. Ndio hapo unajikuta umeingia kwenye Kundi baya la watu wasiojitambua ama makundi mabaya ya nguvu za giza.

Unapokuwa umepiga hatua yoyote kwenye maisha yako, usijaribu kukaa kitako na Kuanza kujipongeza ama kupuuza hatua ndogo ndogo ulizopitia ama waliokusadia huko nyuma na ukajisahau ukaanza kujipongeza na kujisahau utafulia.


Ama ukajiamini kupita kiasi na ukajiona ‘Umewini’  utafulia

Kila hatua unayopitia ikakuletea senti kadhaa unatakiwa uwekeze muda wako,maarifa na akili yako  hapo,  kama ni kwenye ajira, heshimu ajira yako, kama ni kwenye kilimo heshimu kilimo chako na mazao.

Yako na kama wewe ni MJASIRIAMALI waheshimu wateja wako. Usipowaheshimu wateja wako utakuwa unataka kubugia faida badala ya kuigusa jamii ambao ndio msingi mkubwa wa mjasiriamali.

Utagundua kwamba waliofanikiwa hawapo huko kwenye sayari mpya ya Proxima Centauri.

Wakati fulani nilipokuwa nikijifunza jinsi ya kuwekeza kwenye ARIDHI nje ya mji, Nilifika kijiji cha  Ihalimba Kilomita zaidi Ya 66 kutoka Mafinga mjini, Nilisikia na kusimuliwa habari ya ndugu mmoja aliyekuwa ameanzisha  duka kubwa sana la jumala na rejareja. Miaka ya mwanzo alifanikiwa sana na kujaza wateja wengi sana kiasi cha kushangaza watu wa kijiji hicho na baadae alipoona wanakijiji wote ni wateja wake, akaanza dharau kubwa kwa wateja….Mpaka juzi ninapita pale Ihalimba jengo la duka hilo limegeuzwa kuwa saluni ya kunyoa kwa kutumia wembe aina ya ‘Topaz’

Waliofanikiwa hawaishi kwenye sayari mpya ya Proxima Centauri.Tupo nao ni wanyenyekevu na wasikivu na hufuata kanuni za mafanikio na wengi wao hawakufika shule kabisa, ama waliishia njiani.

Na Hii ndio tafakari yetu ya Leo.
Ni mmmi MWANA GoBig mwenzako Meshack Maganga. LEKICHARA wa Mpango wa Elimu kwa waliokimbia Umande Yaani MEKU lakini nikajielimisha kwa kujifunza kwa Wakimbia umande wenzangu.

Meshackmaganga@gmail.com

read more at http://meshackmaganga.co.tz/2016/10/04/waliofanikiwa-hawaishi-kwenye-sayari-ya-proxima-centauri/
Previous
Next Post »