MESHACK MAGANGA: Kilimo cha miti ni mgodi wa kiuchumi


Na: Markus Mpangala
 IMEZOELEKA kuwa katika jamii yetu mafanikio yanaweza kupatikana kwa njia ya kutafuta ajira mara baada ya kutimu masomo. Lakini kwa Meshack Maganga ambaye ni mkazi wa Iringa hali imekuwa tofauti na amedhihirisha kuwa msomi yeyote anaweza kuleta mabadiliko ndani ya jamii bila kutafuta ajira serikalini ama popote. Pia anadhihirisha kuwa maisha yanapatikana mahali popote si lazima kuishi maeneo ya mjini.

Fuatilia mahojiano haya;- MTANZANIA: Mkoa wa Iringa unasifika kwa kilimo cha miti ambazo hutumika kwa nguzo za umeme, mbao, hewa ya ukaa na kadhalika.
 Meshack Maganga, wewe ni miongoni mwa wanaojihusisha na kilimo cha miti, ulianza lini shughuli hii na nini kilikuvutia?
MAGANGA: Kabla sijaanza kilimo cha miti, nilianza na kilimo cha mboga mboga mwaka 2011, (baada ya kuhitimu masomo ya chuo kikuu hapa, Iringa), katika kijiji cha Kalenga, pia nilianza kufuga kuku Iringa mjini, baada ya hapo kaka yangu alianza kunihimiza na kunihamasisha kuhusu kilimo cha miti, wakati huo yeye alikuwa akijihusisha na kilimo hicho. Nilibahatika pia kukutana na Rais wa wapanda miti mkoani Iringa Mzee Chang’a (Rich Dad) ambaye alinifundisha kilimo cha miti na kunipatia hamasa kubwa sana na pia alinisaidia kupata miche. Na baadaye nikaanza ushirikiano na rafiki yangu Albert Sanga ambaye anajishughulisha sana na kilimo cha miti. Baada ya kupata pesa mwaka huo, nilinunua shamba la ekari 10 na kuzipanda miti ya mbao kutokana na pesa niliyopata baada ya kuuza matango niliyolima kijijini Kalenga. Nikaongeza bidii zaidi ya kulima matango na kununua mashamba mengi zaidi, mpaka mwaka huu 2013, tayari nilikuwa nimenunua ekari za kutosha zenye miti ndani. Lengo langu ni kubwa sana, nimepania kuwa na ekari nyingi zaidi zenye miti itakapofika 2018. Pamoja na kuungana na serikali na dunia kwa ujumla katika kulinda mazingira, ninakithamini kilimo cha miti katika eneo hili ili kujiandaa kiuchumi kwa faida yangu na jamii inayo nizunguka. Nina malengo ya kugugusa jamii. Kwa hiyo huu ni mwaka wa tatu tangu nilipo jiajiri kwenye kilimo cha miti.

MTANZANIA: Unaweza kuwaeleza wasomaji wetu na watanzania kwa ujumla juu ya faida ya kilimo cha Miti?
 MAGANGA: Kilimo cha miti, kina faida sana, pengine baadhi ya watanzania wa ndani na nje ya nchi wengi wao hawajabahatika kusikia faida ya kilimo hiki, ama wengi wao wamekisikia na kuzifahamu faida za kilimo cha miti. Wanashindwa waanzie wapi, na ndio maana mpaka sasa wanaolima miti ni watanzania wachache sana, na wale waliojitokeza kulima miti ndio mamilionea wa miaka michache ijayo. Mwaka jana nilitoa somo la “Usikubali kuwa mnyonge wa kiuchumi ndani ya Tanzania” kama njia ya kuhamasisha kilimo cha miti. Nilisema kuwa Kilimo cha miti ya mbao, nguzo, milunda na miti ya kuni na dawa, kimepata umaarufu wa ghafla miaka ya hivi karibuni kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ongezeko la mahitaji ya mazao ya miti na changamoto ya mazingira. Hapa nchini mkoa wa Iringa ni moja ya mikoa maarufu inayoongoza kwa misitu mikubwa ya kupandwa. Miti inatumika kwa mbao, nguzo za umeme, nguzo za kujengea pamoja na utengenezeaji wa karatasi na madawa. Hivi sasa kumeibuka fursa nyingine mpya ambapo mashirika ya kimazingira kutoka Magharibi yananunua hewa ya ukaa. Kwa maana hiyo unaweza kupanda shamba la miti halafu ukawa unakusanya dola kwa kuuza hewa ukaa wakati ukisubiri miti ikomae uvune mbao, nguzo ama miti ghafi ya kutengenezea karatasi. Hii ni sawa na kutengeneza pesa ukiwa umelala nyumbani kwako (Making money while sleeping). Mbali na kuuza hewa ukaa, vile vile unaweza kufuga nyuki na kuendelea kuvuna asali.
MTANZANIA: Kuna changamoto gani katika kilimo cha miti na uchumi kwa ujumla?
MAGANGA: Nimekutana na changamoto nyingi sana baadhi ya changamoto nilizo kutana na nazo tangu nilipoanza kilimo cha miti; kukosa pesa za kutosha hasa kipindi cha kupanda miche mipya kinapoaanza, maana unapopanda miti mpya unatakiwa uwe na pesa ya kutosha. Changamoto nyingine ni tatizo la usafiri, mashamba mengi ya miti yapo nje ya mji wa Iringa, unatakiwa usafiri kilomita nyingi kwa siku mpaka kufika sehemu yalipo mashamba hasa katika wilaya ya Mufindi na Kilolo, wakati wa masika kama haya barabara haipitiki kwa sehemu kubwa. Pia kuna changamoto ya moto wa msituni, kipindi cha nyuma kabla ya ujio wa makampuni makubwa yanayojihusisha na kilimo cha miti, kulikuwa na tatizo kubwa la moto kuchoma baadhi ya mashamba, lakini kwa sasa wananchi wameelimika sana, hakuna tena tatizo la moto kama zamani, moto ukitokea ni ule moto wa bahati mbaya. Lakini changamoto hii kwangu ilikuwa fursa, sikurudi nyuma mpaka leo naona mafanikio.

MTANZANIA: Umeeleza awali kuwa ni watanzania wachache sana wanajihusisha na kilimo cha miti. Lakini una ushauri gani kwa kwao na watanufaikaje kiuchumi kupitia kilimo cha miti?
MAGANGA: Vijana wanaoishi mkoani Iringa na Tanzania kwa ujumla na pia vijana watanzania waliokimbilia nje ya nchi, wana nafasi kubwa sana ya kunufaika na uwekezaji kwenye kilimo cha miti, na hapa ninaongelea vijana wa kike na wa kiume, waliomo kwenye ajira rasmi na wale waliojiajiri kama mimi, na wale waliopo masomoni wasibweteke na mikopo wanayoipata huko wanakosoma. Watanzania wanaweza kunufaika na kilimo cha miti kwa aina mbalimbali, lakini ninaweza kuzitaja chache hapa. Unaweza kuamua kuuza miti (magogo) ambapo kwa nguzo kwa mti mmoja uliokomaa vizuri unauzwa kuanzia 80,000/-. Kwa upande wa miti ya mbao na karatasi, iliyokomaa vizuri mti mmoja huuzwa kuanzia 60,00 kutegemeana na umbali wa shamba. Shamba linapokuwa mahali kusikofikika bei ni ndogo zaidi). Namna ya pili ya uvunaji ni kuvuna mwenyewe kwa maana ya ama kupasua mbao au kutengeneza nguzo za umeme za kuuza. Mvunaji inakulazimu uwe katika biashara kamili ya mbao kwa sababu utahitaji mashine, leseni, vibali na taratibu nyingine,na hapa ndio penye faida kubwa sana. Soko la mbao na nguzo/mirunda liko juu sana na uhitaji wake ni mkubwa kuliko uzalishaji. Nadhani unatambua kuwa mahitaji ya bidhaa za miti yameongezeka kwa kasi sana miaka ya hivi karibuni. Hata hivyo kwa mujibu wa tafiti zilizofanyika na wataalamu wakiwemo SUA wanatueleza kuwa soko la bidhaa za misitu (mbao, nguzo n.k) litaendelea kupanda bila kushuka kwa miaka 25 ijayo kuanzia mwaka 2010. Kama wawekezaji tunakuwa kuwa na hamasa chanya katika hilo ijapokuwa hatuachi kuweka tahadhari ya ‘risks’ (hasa market changes) kama ambavyo ni kawaida kwa biashara yeyote duniani.

MTANZANIA: Umeeleza kuna mashirika yananunua hewa ya ukaa. Pia umesema soko la mbao ni kubwa na lina manufaa kwa anayehitaji. Je unadhani kitu gani kinaweza kusaidia kubadilisha fikra za watanzania kuelewa faida itokanayo na kilimo cha Miti?
MAGANGA: Kwa sasa dunia imebadilika sana na itaendelea kubadilika, iwapo sisi tutajifanya hatuyaoni mabadiliko hayo na kuendelea na mitazamo ile ile ya zama za kati za mawe, ikumbukwe kwamba, janga kubwa duniani si kifo wala ajali, bali ni kuishi bila malengo. Vijana wadogo wake kwa waume wanaohitimu vyuo mbalimbali wapo bize kusaka ajira, na wale ambao bado wapo shuleni na vyuoni na wao wana ndoto za kupata ajira (idadi yao ni kubwa sana).
Na baadhi ya waliopo kwenye ajira wamechoshwa na ajira zao,wanafokewa kama watoto, wanakosa muda wa kufanya mambo yao, na wengine wanalalamikia mishara midogo. Serkali imetoa fursa kwa wananchi kumiliki ardhi na msisitizo upo kwenye kilimo lakini bado wengi wao wanaona kilimo ni kama kazi ya watu wasio soma na waliokosa cha kufanya, wanaona bora watembeze bahasha kuomba kazi ambazo kwa hakika ni chache sana kuliko kujiajiri.
Mbaya zaidi waliopo kwenye ajira wake kwa waume, wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea hawapo tayari kuachia ajira zao. Unajua ni kwanini hawataka kuachia ajira zao? Bado wanajiandaa, na wengine hawajapata mitaji miaka nenda rudi. Kwanini usiwekeze kwenye kilimo cha miti? Pale mkoani Morogoro kuna fursa ya kilimo cha Mitiki, Tanga kuna fursa ya kilimo cha miti ya mbao, Ruvuma na kwingineko, ama tunasubiri ardhi iishe ndio tuanze maneno? Rafiki yangu, Albert Sanga, aliwahi kusema Mazoea na utamaduni wa watanzania wengi kudhani kwamba tunaonewa. Mtindo wa kuishi maisha ya kutaka kuhurumiwa yanatupotezea muda wenye thamani.
 Tumekuwa tukilalamika kuwa wageni (wanaokuja kwa jina la wawekezaji) wanatupora ardhi; lakini tusichokitafakari ni hiki, “Mimi kama mtanzania kwa nafsi yangu na kwa uwezo wangu nimefanya nini cha maana katika ardhi ninayoweza kuipata hapa nchini ama ninayomiliki?”.
Kumbuka kuwa dunia haina huruma kwa mwanadamu anaye lala tu huku akilaumu serkali, ama akiendelea kukesha akifanya maombi, bila kufanya maana Mungu hana huruma na watu wavivu ama akiendelea kuwalaumu wazazi wake ama kozi aliisoma chuo kikuu, ama akimsingizia shetani kila kukicha. Mtanzania yeyote wa kada yoyote atakayependa kuungana na sisi katika kilimo cha miti ili kutunza mazingira wakati tunasubiri kuvuna miti, tunamkaribisha Iringa aje kujifunza kwenye mashamba yetu kisha atafanya maamuzi.

 Nimekuwa nikirudia kauli ya Baba yangu (Mwenyekiti wa wapanda miti-Iringa) maarufu kama ( Rich Dad) ambaye siku za karibuni amepewa Tuzo ya Rais kwa kuwa mpandaji namba moja wa miti na utunzaji wa mazingira. Kila mwanzo wa msimu wa kupanda miti amekuwa akitoa msaada kwa watanzania wa ndani na nje ya Tanzania kuwasadia kupata eneo la kupanda miti na miche. Watu wasikubali kuwa wanyonge wa kiuchumi ndani ya Tanzania.
Previous
Next Post »