ACHOMWA KISU, AFIA POLISI:KISA DENI LA SHILINGI ELFU TANO,MTUHUMIWA AKAMATWA AACHIWA!!



INATISHA sana! Renard Mabula, mkazi wa Kiluvya jijini Dar es Salaam amekufa ndani ya Kituo cha Polisi cha Gogoni, Kinondoni jijini Dar es Salaam baada ya kukimbilia hapo kufuatia kuchomwa kisu tumboni na mtu aliyetajwa kwa jina la Moleli (22), Uwazi lina mkanda kamili.

Kwa mujibu wa habari za kipolisi, tukio hilo lilijiri Februari 11, mwaka huu, Gogoni ambako ndiko kwenye makazi ya mtuhumiwa na marehemu huyo.
Awali ilidaiwa kuwa, marehemu huyo alikuwa akidaiwa shilingi elfu tano na Moleli lakini alikuwa akimzungusha kwa muda mrefu bila kumlipa.
“Siku ya tukio, Moleli alikwenda kwa marehemu kumdai fedha zake hizo na kujibiwa kuwa, kwa muda ule hakuwa na kitu ndipo, Moleli akaamua kumchoma kwa kisu tumboni.
“Marehemu kuona vile huku akivuja damu kwa wingi alikimbilia Kituo Kidogo cha Polisi cha Gogoni Kiluvya. Alipofika alisimulia mkasa wake lakini alipomaliza tu akakata roho, mwili wake ukapelekwa Hospitali ya Tumbi, Kibaha, Pwani ambapo madaktari walithibitisha kuwa alishafariki dunia,” kilisema chanzo.
Katika hali isiyokuwa ya kawaida, baba mzazi wa mtuhumiwa huyo (jina tunalo) alisema analishangaa sana Jeshi la Polisi Kituo cha Mbezi ambapo mtoto wake alipelekwa kutoka kituo kidogo cha Gogoni baada ya kutuhumiwa kwa mauaji ya Mabula lakini aliachiwa huru.
Akaendelea: ‘’Mimi mwenyewe huyo mtoto wangu alishawahi kunitishia kuwa atanichoma kisu baada ya kumtaka aende shule. Tumemshauri mara nyingi na mama yake lakini hataki kusikia, sijui ni mtoto gani asiyesikia wazazi?’’ alihoji baba huyo.
Wakati hayo yakitokea, mwanamke mmoja wa eneo hilo aliyejitambulisha kwa jina la Getruda Athanas (36), yuko shakani akidai kwamba, Molel amekuwa akimtishia kumchinja kwa kisu baada ya kumtuhumu kuiba kuku wake.
Mwanamke huyo alikimbilia Kituo cha Polisi Gogoni na kufungua malalamiko kwa kumbukumbu KLV/RB/521014 KUTISHIA KUUA KWA MANENO.
Akizungumza na Uwazi, Getruda alisema: “Nilipomuuliza kama kweli aliiba kuku wangu, alikiri akidai alitaka apate fedha. Lakini akaniambia nikiendelea kumfuatilia atanichinja, akitoa mfano wa jinsi alivyomuua Mabula kwa kisu.”
Uwazi  lilimtafuta Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, ACP Camilius Wambura na kumuuliza kuhusu taarifa hizo ambapo alikiri.
Uwazi: Sasa afande ililkuwaje mtuhumiwa akakamatwa na kuachia huru?
Kamanda: Nimeshamwagiza kamanda  wa polisi wa wilaya ‘OCD’ (hakumtaja jina) kufuatilia madai ya mtuhumiwa kuachiwa huru.
Previous
Next Post »