.Watu 11 zaidi wauawa Tana River

Takriban watu kumi na mmoja wameuawa katika mapigano zaidi katika eneo la Tana River Kusini Mashariki mwa Kenya.

Ripoti zinasema miongoni mwa waliouawa katika shambulio hilo lililotokea alfajiri ya siku ya Alhamisi ni watoto watano.



Uchunguzi wa awali umebainisha kuwa shambulio hilo ni la kulipisa kisasi mauaji yaliyotokea katika eneo hilo usiku wa kuamkoa siku ya Jumatano dhidi ya watu wa jamii wa Orma.

Watu wengine tisa waliuawa siku ya Jumatano pale wapiganaji wa Pokomo walipoishambulia kijiji kimoja cha watu wa Orma na kutetekeza nyumba na kuiba mifugo.

Kulipisa kisasi


Wengi wa waliojeruhiwa wakati wa shambulio hilo ni watu wa kabila la Orma.

Walionusurika shambulio hilo wanaendelea kutibiwa katika hospitali kadhaa kutokana na majeraha ya risasi, panga na moto.

Shirika la Msalaba Mwekundu limesema kuwa watu waliokuwa wamejihami kwa silaha walivamia kijiji cha watu wa Orma na kuwaua watu sita.

Shambulio hilo katika kijiji cha Kibusi linajiri siku moja baada ya shambulio lingine lililotokea jana katika kijiji jirani ambako watu wengine sita waliuawa.

Kwa mujibu wa shirika hilo, vijiji hivyo viko umbali wa kilomita ishirini na kuna kituo kimoja cha polisi katikati.

Zaidi ya mia moja waliuawa katika mashambulio kama hayo mwaka uliopita na hali ya usalama katika eneo hilo umeimarishwa.

Watu wa jamii hizo mbili walikabiliana mwezi Agosti mwaka uliopita baada ya watu wa jamii ya Ormo kushutumiwa kulisha mifugo wao katika mashamba ya watu wa jamii ya Pokomo.
Previous
Next Post »