Wagonjwa wa Saratani Ocean Road kunufaika na huduma za TEKNOHAMA


   
Vodacom Tanzania Foundation yatoa msaada kufanikisha mchakato huo
Wahanga wa ugonjwa wa Satarani wanaotibiwa katika taasisi ya Uchunguzi wa Saratani ya Ocean Road iliyopo jijini Dar es Salaam wataanza kunufaika na huduma bora kwa njia ya kisasa kwa kutumia Teknolojia ya Mawasiliano kutokana na mchakato wa serikali kuimarisha huduma za taasisi hiyo.
Wakati jitihada hizo za serikali zinaendelea sekta baadhi ya sekta binafsi zimeanza kuunga mkono jitihada hizo za serikali ambapo kampuni ya mawasiliano ya Vodacom kupitia taasisi yake ya kuhudumia masuala ya kijamii imetoa msaada wa kompyuta 10 za kisasa kwa taasisi hiyo.
Akiongea wakati wa kupokea msaada huo katika hafla iliyofanyika hospitalini hapo leo,Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo,Dk.Julius Mwaiselage,amesema kuwa msaada huu umepatikana katika kipindi mwafaka ambapo hospitali hiyo iko katika mchakato wa kuendesha huduma zake kidigitali.
Dk.Mwaiselage alisema kuwa hivi sasa kumekuwepo na ongezeko kubwa la wagonjwa wanaofika hospitalini hapo kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na kutibiwa hivyo kuna umuhimu mkubwa kuhakikisha kuwa ili kuwahudumia ni kuwa na huduma za kisasa katika kila idara kwa njia ya TEKNOHAMA na tayari serikali na wadau mbalimbali wameanza kufanikisha mchakato huo.
Aliishikuru kampuni ya Vodacom kwa kuwa mstari wa mbele kuunga mkono jitihada hizo “Tunawashukuru Vodacom Tanzania Foundation kwa kuunga mkono jitihada za kuboresha huduma zetu ili ziweze kuwa bora zaidi na tunatoa wito kwa taasisi nyingine kuendelea kutuunga mkono katika mapambano haya ya kutokomeza ugonjwa wa Saratani nchini na kuwapatia huduma bora wahanga wa ugonjwa huu”.Alisema.
Kwa upande wake Mkuu wa Mawasiliano na Uhusiano wa Vodacom ,Jacquline Materu,alisema kuwa Vodacom kupitia taasisi yake ya kuhudumia jamii ya Vodacom Tanzania Foundation imekuwa mstari wa mbele kuunga mkono jitihada za serikali kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo kwenye jamii hususani katika kuboresha sekta ya elimu na afya.
“Leo tuko hapa kutoa msaada wa kompyuta 10 lakini tumekuwa tukishiriki kufanikisha miradi mbalimbali ya afya ambayo imesaidia kuokoa Maisha ya watanzania wenzetu hususani Wanawake na watoto wachanga na tutaendelea kuunga mkono  jitihada za serikali kuboresha Maisha ya watanzania “.Alisema.
Materu aliitaja baadhi ya miradi hiyo kuwa ni mradi wa ambulance wa kuwawahisha akina mama wajawazito katika vituo vya afya wanapokaribia kujifungua,mradi wa kugharamia  uchunguzi na matibabu wa akina mama wahanga wa Fistula na Saratani,Mradi wa kusaidia vifaa kwa watoto wanaozaliwa kabla ya umri na kufanikisha mafunzo mbalimbali ya watumishi wa kada ya afya.
Mbali na kutoa msaada wafanyakazi wa Vodacom pia wamekuwa wakijitolea muda wao kushiriki kusaidia miradi ya kijamii katika sekta ya afya ikiwemo kutembelea mahospitalini na kutoa misaada kwa wagonjwa na kuwapatia faraja.

Kwa upende wao baadhi ya wagonjwa waliolazwa hospitalini hapo kupata matibabu wameshukuru  wafanyakazi wa Vodacom kwa msaada na kuwatembelea kwa ajili ya kuwapatia faraja.


Previous
Next Post »