Rudisha hatashiriki mbio za dunia Moscow

David Rudisha wakati wa michezo ya Olimpiki mjini London

Bingwa wa Olimpiki na dunia na mshikilizi wa rekodi ya ulimwengu katika mbio za mita mia nane kwa wanaume mkenya David Rudisha, amejiondoa kutoka kwa mashindano yajayo ya dunia yatakayofanyika mjini Moscow Mwezi Ujao.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotumwa kwa vyombo vya habari, na naibu makamu wa rais wa shirikisho la mchezo wa riadha nchini Kenya, David Okeyo, Rudisha hatalitetea taji lake mwaka huu kutokana na jeraha.

Okeyo amesema baada ya kushauriana na mwanariadha huyo pamoja na makocha wake, imebainika kuwa Rudisha bado angali anauguza jeraha na haitakuwa vyema kwake kushiriki katika mashindano hayo kwa kuwa inaweza kuhatarisha zaidi jeraha hilo.

''Nasikitika sana kuwa siwezi kuteteza taji langu la mita mia nane mjini Moscow. Jeraha langu la mguu halijapona kwa wakati ufaao ili kuniwezesha kushiriki katika fainali hizo za dunia. Kwa hivyo nawatakia wanariadha wenzangu kila la heri katika mashindano hayo ya dunia yatakayofanyika mjini Moscow.'' Amesema Rudisha.

Previous
Next Post »