Baraza jipya la mawaziri latajwa Japan

Shinzo Abe


Waziri mkuu mpya wa Japan, Shinzo Abe, ametangaza baraza lake jipya la mawaziri, huku akianza majukumu ya kuimarisha uchumi wa taifa hilo.

Baraza hilo la Mawaziri lilitanagzwa muda mfupi baada ya bunge la nchi hiyo kumuidhinisha Bwana Abe kuwa Waziri Mkuu, kufuatia ushindi wa chama chake katika uchaguzi mkuu mapema mwezi huu.

Chama cha Liberal Democratic na mshirika wake wana zaidi ya wabunge theluthi mbili katika bunge la wawakilishi

Bwana Abe, ambaye alikuwa waziri mkuu mwaka wa 2006-07, amemteua aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiy Taro Aso, kuwa waziri wa fedha.

Wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanasema, baraza hilo la mawaziri linajumuisha washirika wa karibu wa Bwana Abe, huku akianza mikakati ya kunusuru uchumi wa taifa hilo.

Aliyekuwa waziri wa Biashara na Viwanda Akira Amari, ameteuliwa kuwa waziri anayehusika na masuala ya uchumi naye mwanasiasa mkongwe Toshimitsu Motegi ameteuliwa kuwa waziri wa biashara.


Inakisiwa kuwa waziri huyo atakabithiwa jukumu la kubuni sera mpya kuhusu nishati kufuatia mkasa wa nuklia wa Fukushima uliotokea mwaka uliopita.

Bwana Abe, anakisiwa kuwa mwanasiasa asiyeegemea upande mmoja lakini aliondolewa madarakani baada ya umaarufu wake kushuka na alijiuzulu kutokana na matatizo ya kiafya.


Yoshihiko Noda
Aliyekuwa Waziri mkuu wa Japan Yoshihiko Noda

Lakini anarejea tena madarakani wakati mgumu na anakuwa Waziri Mkuu wa saba wa Japan, katika kipindi cha miaka sita.

Abe ambaye ni mjukuu wa aliyekuwa waziri kuu wa nchi hiyo na mwanawe aliyekuwa waziri wa mambo ya nje, amehaidi kuchukua msimamo mkali kuhusu mzozo wa mpaka na nchi jirani ya Uchina.

Serikali ya Uchina, imetoa wito kwa serikali mpya ya Japanm kuchukua maamuzi yanayoweza kutekelezwa kushughulikia mzozo kuhusu umiliki wa visiwa vya Mashariki ya Bahari ya Uchina.

Bwana Abe pia ametoa wito wa kuifanyia marekebisho katiba ya nchi hiyo na kujumuishwa kwa vipengee kuhusiana na uzalendo.

Chama cha LDP kilishinda chama tawala cha Democratic Party-DPJ katika uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 16 mwezi huu.

Kiongozi wa chama hicho cha DPJ Yoshihiko Noda, alijiuzulu baada ya chama chake kushindwa.
Previous
Next Post »