SUNZU KUKIMBILIA CHINA MKATABA WAKE NA SIMBA UKIISHA

MSHAMBULIAJI Felix Sunzu huenda akatimkia nchini China kucheza soka la kulipwa baada ya mkataba wake na Simba kumalizika.
Mzambia huyo anaamini kuwa kucheza Ligi ya China itamsaidia kuimarisha zaidi kiwango chake kurudisha makali yake ya kuzifumania nyavu timu pinzani.
Awali Sunzu alikuwa tegemeo katika kikosi cha timu ya taifa ya Zambia 'Chipolopolo' na Watanzania wanamkumbuka alipoibuka mfungaji bora wa mashindano ya Cecafa 2010 jijini Dar es Salaam.
Lakini tangu alipojiunga na Simba 2010 akitokea FC Lupopo ya DR Congo ameshindwa kurejea kwa mara nyingine katika kikosi cha timu ya taifa ya Zambia.
"Nina mpango wa kwenda China mara tu mkataba wangu na Simba itakapoisha." alisema Sunzu.
"Wakala wangu ndiye mwenye jukumu la kushughulikia dili hilo kwa sasa."
"Naipenda Simba kwa sababu nimeishi vizuri na yanayotokea ni mambo ya kawaida tu."
"Naendelea na mazoezi yangu binafsi ili kujiweka vizuri ingawa mazoezi ninayoyafanya peke yangu hayaniweki fiti zaidi na itakuwa vizuri kama timu ikirudi niungane nao ili tumalizie mechi hizo zilizobaki. alisisitiza.
Previous
Next Post »